Fahamu Vyakula Vinavyotuua Kimyakimya Katika Mazingira Tunayoishi

Tukumbuke kwamba uzima wa mtu unategemea sana kinga aliyonayo mwilini,kinga ambayo hujengwa na ulaji wa vyakula vyenye virutubisho vya aina mbalimbali. Kwa namna ambavyo Mungu ametuumba, mwili unapaswa kujilinda wenyewe dhidi ya maradhi ya kila aina. Ukiwa na kinga imara ya mwili siyo rahisi kuugua mara kwa mara. Magonjwa yanayojitokeza haraka pale kinga ya mwili inapokuwa chini, ni pamoja na kuugua malaria mara kwa mara, kifua kikuu, kutokwa na majipu, kutokwa uvimbe wa ajabuajabu katika mwili, kupatwa na mkanda wa jeshi, kupatwa na saratani na magonjwa mengine ya maambukizi.

Je, Chanzo Cha Kushuka Kwa Kinga Mwilini Ni Nini?

Ili uwe na kinga imara ya mwili, ni lazima uwe unakula mlo kamili unaojumuisha matunda, mboga za majani, nafaka na vyakula vingine vya asili, kwa sababu kila unachokula kina faida yake mwilini. Lakini siyo tu kula chochote kinachoitwa ‘chakula’, bali ule kilichosahihi. Katika maisha tunayoishi sasa, hasa mijini, idadi Kubwa ya watu hawali kabisa vyakula sahihi, badala yake wanakula vyakula ambavyo si tu ni hatari kwa afya zao, bali pia hudhoofisha kinga ya asili ya mwili na hivyo kuufanya mwili kubaki dhaifu na unaoweza kupatwa na ugonjwa wowote. 

NUKUU:  Chanzo kikuu cha kushuka kwa kinga ya mwili kinasababishwa na ulaji wa vyakula visivyo sahihi ambavyo ndivyo vinavyopatikana kwa wingi kila mahali, hasa sehemu za mijini. Vyakula visivyofaa ndivyo vinavyotangazwa na kunadiwa kwenye vyombo vya habari kuwa bora. 

1. Unga Wa Ugali

Unga wa ugali unaotumiwa na watu wengi nchini ni sembe nyeupe. Chakula kikuu katika kaya nyingi zinazotumia ugali kama mlo wa kila siku huwa ugali mweupe uliotokana na mahindi yaliyokobolewa na kusafishwa, kisha kusagwa na kutoa unga safi mweupe. Kwa mtizamo wa macho na ladha ya mdomoni, wengi wanaamini kuwa ugali wa aina hii ndiyo mzuri na unaotakiwa kuliwa. 

NUKUU: Ulaji wa ugali wa aina hii hauna faida yoyote mwilini, kwani hauna virutubisho,kwa sababu vilishaondolewa vyote wakati wa kukoboa. Virutubisho muhimu vya muhindi viko kwenye kiini chake, hivyo unapokiondoa unakuwa umeondoa lishe muhimu. Ndiyo maana hata panya hawali mahindi yaliyokobolewa. Kwa faida ya afya zetu na kwa ajili ya kuimarisha kinga ya miili yetu, sote tunatakiwa kula ugali wa dona, mtama au ulezi kabla hata ya kuugua. Vyakula hivi ni muhimu sana na siyo vya kimasikini kama ambavyo watu wengi wanadhani. Kwa bahati mbaya, upatikanaji wa unga wa dona umekuwa mgumu na ghali kuliko sembe nyeupe, hivyo kuwafanya watu wengi kukimbilia sembe nyeupe ambayo inapatikana kirahisi kila kona ya nchi na kwa bei nafuu. Kwangu mimi naliona tatizo hili ni la kitaifa na kisera.

Je, Ulaji Wa Matunda Na Mboga Una Faida Gani?

Hakuna kitu muhimu kwa mwili wa binadamu kama kujenga kinga ya mwili. Mwili unapokuwa na kinga imara, si rahisi kuugua magonjwa ya ajabu. Miongoni mwa kazi nyingi za matunda na mboga za majani, ni pamoja na hiyo kazi ya kujenga mwili na kuujengea uwezo wa kujikinga wenyewe. Pamoja na umuhimu huo, ni watu wachache sana hula matunda na kuyachukulia kama sehemu ya milo yao ya kila siku. Watu wengi hula matunda au mboga za majani ‘kwa bahati mbaya’, huona siyo chakula muhimu sana. 

NUKUU: Hili ni kosa kubwa miongoni mwa makosa mengi yanayofanywa na watu katika masuala ya afya. Matunda yanatakiwa kuliwa kila siku na kwa wingi, vivyohivyo mboga za majani. Unapoacha kula matunda na mboga za majani za aina mbalimbali, jua unaukosesha mwili wako kinga dhidi ya maradhi yanayoweza kujitokeza mwilini. 

Je, Ni Vyakula Gani Vinavyotumaliza Kwa Kasi Zaidi?

Vyakula tunavyotakiwa kuvila, hatuvili tena na pengine upatikanaji wake ni wa shida, hivyo tunalazimika kula vilivyopo licha ya kuwa vina madhara kwa afya zetu. Hali hii imeongeza idadi ya wagonjwa na magonjwa sugu. Chakula kikuu cha mijini ni chips, kuku, mayai, soda, juisi za makopo au paketi, nyama choma na pombe. Pia kuna mkate mweupe, maandazi na chapati. Vyakula hivi huliwa kila siku, lakini ukivichambua utagundua havina faida yoyote mwilini zaidi ya kuingia na kutengeneza maradhi.

2. Chips

Chips ambayo kwa kawaida hutengenezwa kutokana na viazi mviringo na kukaangwa kwenye mafuta, ni chakula kinachotakiwa kuliwa kwa kiasi kidogo na kwa nadra sana, kwa sababu kiko kwenye kundi la vyakula vyenye mafuta mengi ambavyo huliwa kwa uchache sana. Lakini hali halisi ni kinyume chake. 
Watu wengi ambao wamekuwa wakitumia ulaji wa chips hasa walioko mijini, vyuoni au mitaani, ndio wamekuwa wakipatwa na magonjwa mbalimbali hasa katika madhaifu ya nguvu za kume, mbegu za mwanaume kuwa nyepesi, kupatwa na fangasi sehemu siri kwa wanawake, nk. 

3. Kuku Wa Kisasa

Kwa kawaida, kuku wengi wanaotumika kwenye biashara ni kuku wa kizungu. Nyama ya kuku hawa haina virutubisho sawa na kuku wa kienyeji. Hii inatokana na ukweli kwamba kuku wa kizungu hulishwa madawa mbalimbali ya kuwakinga na magonjwa na hulishwa vyakula vilivyochanganywa madawa ili wakue upesi. Kwa mazingira hayo, nyama itokanayo na kuku wa aina hii haiwezi kuwa bora. 

NUKUU: Kiasili kuku huishi mazingira huru kwa kula vyakula ambavyo hujenga na kuukinga mwili wake dhidi ya magonjwa mbalimbali, kuku wa aina hii ndiye anayefaa kuliwa na kuleta faida ya nyama ya kuku inayokusudiwa.

4. Mayai Ya Kuku Wa Kisasa

Halikadhalika, mayai yanayopatikana kwa wingi mijini ni yale yatokanayo na kuku wa kufuga. Kiasili, mayai ya kuku wa kufuga, hayawezi kuwa sawa na mayai yatokanayo na kuku wa kienyeji. Huhitaji kuwa mwanasayansi kuona tofauti kati ya yai la kuku wa kienyeji na kuku wa kufuga, kwani mayai hayo yakipikwa huwa tofauti kwa ladha na hata rangi. 

NUKUU: Ni ukweli ulio wazi kuwa kuku wa kufugwa hulishwa vyakula vya kutengeneza ambavyo ndani yake huwekwa kemikali na madawa mbalimbali, wakati kuku wa kienyeji hula vyakula asili kwa kujitafutia wenyewe na mazingira wanayoishi ndiyo yanayowafanya wawe tofauti na bora. Hivyo ni dhahiri kwamba mayai tunayokula ya kuku wa kizungu yana madhara zaidi kuliko faida mwilini.

5. Soda

Moja ya vinywaji vinavyopendwa na kutumiwa na watu wengi ni pamoja na soda. Matangazo mengi ya biashara yanafanyika kutangaza kinywaji cha soda na kuonesha kuwa ni kinywaji ambacho hakina madhara kabisa kwa mtumiaji. Kwa matangazo hayo na kampeni hizo, familia nyingi zimeamini kuwa soda ni kinywaji bora na hata watoto wetu wamerithishwa imani hii. 

NUKUU: Lakini kwa upande wa pili wa kinywaji hiki, siyo kinywaji salama kama ambavyo imekuwa ikielezwa. Siwezi kusema moja kwa moja kuwa mtu huruhusiwi kabisa kunywa soda kama vile ni sumu, lakini watu walitakiwa kuelimishwa na kuelezwa madhara ya kupenda kunywa soda na athari anazoweza kuzipata mtu kiafya. Naamini tahadhari inayotolewa kwa wanywa pombe, hata kwa wanywa soda ilipaswa kutolewa pia.

6. Juisi Za Chupa Au Kopo

Je, Juisi Yaweza Kuwa Chanzo Mojawapo Cha Kumfanya Mtu Akapungukiwa Na Kinga Mwilini?

Katika hali ya kawaida, juisi ni kinywaji baridi kisicho na kilevi wala madhara kwa mnywaji. Lakini utakuwa sahihi ukizungumzia juisi zilizotengenezwa kwa matunda halisi bila kuongezewa vitu vingine. Katika zama hizi, hali iko tofauti, juisi nyingi tunazodhani ni vinywaji baridi visivyo na madhara kwa afya zetu na za watoto wetu, hali haiko hivyo. Juisi nyingi zinazouzwa kila sehemu ni feki. Ni jambo la kusikitisha kuona jinsi binadamu anavyojaribu kushindana na Mungu kwa kutengeneza vitu vinavyofanana na vile alivyoumba Mwenyezi Mungu kwa ajili yetu. 

NUKUU: Juisi nyingi hutengenezwa kwa kuchanganya maji, sukari na rangi zilizotengenezwa kwa kemikali mbalimbali zikiwemo zenye ladha ya matunda. Juisi za aina hii ndiyo nyingi na zinapatikana kila kona , waathirika zaidi wakiwa watoto wetu ambao hupenda kunywa kwa kufuata utamu wa sukari nyingi zilizowekwa na ladha za matunda. Utafiti umeonesha kemikali (Additives) zinazowekwa kwenye vinywaji hivi, hudhoofisha kinga ya mwili na huwa chanzo cha magonjwa ya saratani na mengine hatarishi. Nakusihi kuacha kunywa kabisa juisi hizo na usimpe mwanao, unamuua. Ukiacha hizo juisi zinazotengenezwa kwa kutumia kemikali ‘mwanzo mwisho’, kuna juisi zingine zinazodaiwa kutengezwa kutokana na matunda, zipo za ‘machungwa’, nanasi’, ‘pasheni’, n.k. 

Yapo makampuni pia yanayojitapa kutengeneza juisi zao asilimia 100 kutokana na matunda na kwamba hakuna kinachoongezwa kingine. (100% fruit, No sugar added au No additives, huandika hivyo kwenye maboksi yao au makopo wanayoweka juisi. Hata hivyo, utafiti wa hivi karibuni umeonesha kuwa makampuni mengi yanadanganya walaji. Kwa sababu siyo kweli kwamba hawaongezi kitu kingine katika utengenezaji wa juisi zao za matunda. Imejulikana kuwa huweka vitu vya kufanya juisi ya kwenye boksi au chupa ikae kwa muda mrefu bila kuharibika, halikadhalika huweka vitu vya kuifanya juisi hiyo kuwa na ladha moja.

NUKUU: Acha nikupe mfano. Katika hali ya kawaida, ukichuma machungwa matano ya mti mmoja, lazima yatakuwa na ladha tofauti, yote hayawezi kuwa na ladha sawa japo yote yanatoka mti mmoja. Kwa maana hiyo, kama ukitengeneza juisi kwa kutumia machungwa yaliyochumwa kutoka miti tofauti, ladha ya juisi lazima itatofautina. Lakini utashangaa kuona ladha ya jusi za maboksi zote zinafanana. Wanachofanya ni kuweka ladha moja kwenye utengenezaji wa juisi zao kabla ya kupeleka kwa mlaji. Halikadhalika, juisi ukishaitengeneza, haiwezi kukaa kwa muda mrefu bila kuharibika. Kwa hiyo, ili kuifanya juisi hiyo iweze kukaa kwa muda mrefu bila kuharibika, lazima iwekewe kemikali ya kuihifadhi isiharibike. Kwa kuongezewa vitu hivyo, hata kama Kwa maelezo hayo, hatushauriwi sana kunywa juisi hizo ‘ready made’ kwa sababu zimekosa uhalisia, kwani zina madhara kwa afya zetu, licha ya maelezo na matangazo mazuri tunayopewa na watengenezaji. Badala yake tutengeneze juisi majumbani mwetu wenyewe kwa kutumia matunda halisi ili kupata faida katika miili yetu. Jiepushe na matumizi ya sukari nyingi katika juisi unayoitengeneza mwenyewe, kwani kwa kufanya hivyo utakuwa unaiharibu, weka sukari kidogo sana ikiwezekana acha kabisa.

Neno La Faraja: Muwe tayari siku zote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa heshima. (1Petro 3:15).

Je, unahitaji huduma? Basi wasiliana nasi kwa namba hizi: 0768 559 670/0712 181 626,

Arusha-Mbauda,

Karibu sana!

 

Comments

Popular posts from this blog

Fahamu Mambo Yanayosababisha Uke Kulegea

Aina 9 Ya Vyakula Unavyopaswa Kuviepuka Unapokuwa Na Tatizo La Figo

Mambo 6 Yanayopelekea Mwanamke Kuhisi Maumivu Makali Anaposhiriki Tendo La Ndoa